Somo La 7 | Mgogoro Unaendelea

Somo limetafsiriwa na Mgune Masatu
(Yeremia 9, 10 & 26)
Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2011, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.
Utangulizi: Endapo wewe ni mzazi wa watoto ambao kwa sasa ni watu wazima, je, kuna kipindi ambacho hukujua ufanye nini ili kuwasaidia watoto wako? Mimi nilipitia nyakati hizo. Endapo wewe ni kiongozi wa kanisa, je, kuna nyakati ambazo hujui ufanye nini ili kutatua matatizo ya kanisa? Hata nilipokuwa mtoto mdogo, kuna mitafaruku ambayo sikuweza kuisuluhisha katika familia yangu. Je, tunafanya nini katika hali kama hizo? Jibu la kwanza ni kumgeukia Mungu kwa ajili ya kuomba msaada! Lakini, je, Mungu anakabiliana na hali kama hizo ambapo hawezi kutatua tatizo kwa kuwa anatupatia uhuru wa kufanya uchaguzi? Yeremia anaendeleza maonyo yake kwa watu wa Mungu katika somo letu la juma hili, lakini katika maonyo yake tunapata mwangaza wa namna ya kutatua matatizo yanayoonekana kutowezekana kutatuliwa. Hebu tuzame kwenye somo letu la Biblia ili tujifunze zaidi!

I.                   Mkanganyiko
A.                Soma Yeremia 9:1. Je, umewahi kuangalia chemchemi iliyotengenezwa kwa ajili ya umma na kufikiria kwamba pengine ingetengenezwa ili ifanane na kichwa chako? (Kamwe sijawahi kufikiria hivyo! Lakini, Yeremia anatafakari hivyo.)
1.                  Kwa nini Yeremia anakuwa na mawazo hayo yasiyo ya kawaida? (Amesikitika sana kutokana na watu waliokufa kwa sababu hawakulifuata neno la Mungu. Chemchemi zina maji mengi sana, na anatumia ishara hii (fikiria somo la juma lililopita) kuonesha jinsi ambavyo angependa kulia kutokana na huu upotevu mkubwa.)
A.                Soma Yeremia 9:2. Yeremia ana mawazo gani mengine kuwahusu watu wake? (Angependa kuwapeleka jangwani na kuwaacha huko!)
1.                  Je, jambo hili linaonekana kutokuwa na mwelekeo kidogo kwako? Kwa upande mmoja Yeremia anawalilia watu wake, na kwa upande mwingine angependa kuwatelekeza watu wake jangwani. Je, umewahi kuwa na mawazo kama hayo kwa watu unaowafahamu?
A.                Soma Yeremia 9:3. Yeremia analalamika kwamba watu wanasema uongo, wanajiingiza kwenye dhambi za aina mbalimbali, na hawamkiri Mungu. Endapo hawa wangekuwa watoto wako, je, ungewalilia na pia kutaka kuwaacha jangwani?
I.                   Suluhisho la Mungu
A.                Soma Yeremia 9:7. Suluhisho la Mungu kwa ajili ya watu hawa ni lipi? Nilikuuliza ungekuwa na mwitiko gani endapo watoto wako wangekuwa kama watu ambao Yeremia amewaelezea? (Nikiwa kama mzazi, nimekuwa nikishindwa kutambua jambo sahihi la kufanya katika baadhi ya nyakati. Ninaupenda ukweli ambapo Mungu anasema, “Nitende nini kwa ajili yao?” Anachokifanya Mungu ni “kuwayeyusha na kuwajaribu.”)
1.                  Unadhani inamaanisha nini “kuwayeyusha na kuwajaribu” watu? (Mungu anawaletea watu mambo magumu/machungu.)
1.                  Hii inahusikaje kwa kwatoto wako? (Katika nyakati fulani, tunatakiwa kuwaacha watoto wetu wapitie uzoefu wa matokeo ya maamuzi yao mabaya – na kumwomba Mungu kwamba athari zisiwe za moja kwa moja (za siku zote).)
A.                Soma Yeremia 9:23-24. Mungu ana lengo gani kwa ajili ya watu wake? (Watajivuna kutokana na kumjua na kumwelewa Mungu, na sio kujivuna kutokana na kuwa werevu, matajiri au kuwa na nguvu.)
1.                  Jambo hili linanipa wasiwasi kidogo. Unawezaje kujivuna kwamba unamjua na kumfahamu Mungu? Je, umewasikia watu wanaodai kuzungumza kwa niaba ya Mungu na ukadhani kuwa, “Hivyo sivyo ambavyo ninamfahamu Mungu?” Je, wanadamu hawana uwezo wa kutosha kuyafahamu mawazo ya Mungu? (Nadhani jibu linapatikana kwenye fungu. Tunajivunia wema, utendaji haki na unyofu wa Mungu. Hii ni tofauti na kudai kwa kiburi kufahamu kwa mahsusi jinsi Mungu anavyofikiri.)
1.                  Tunawezaje kutumia maelekezo haya kutatua matatizo katika familia zetu na kanisani kwetu? (Tunaweza tusifahamu cha kufanya (tofauti na kuomba), lakini, tukiwa kama wawakilishi wa Mungu, tunaweza kuwa na uhakika wa kumwakilisha Mungu kwa kuwa wema, watenda haki na wanyofu.)
I.                   Mungu Wetu wa Hali ya Juu
A.                Soma Yeremia 10:1-2. “Ishara za mbinguni” zilizowaogofya watu ni zipi?
A.                Soma Yeremia 10:3-5. Je, ni upumbavu kiasi gani kuabudu sanamu? (Ni upumbavu mkubwa sana. Mungu anasema uliitengeneza, haiwezi kusimama wima, wala kutembea au kuzungumza. Kwa nini utarajiwe kulindwa na kitu ambacho hakiwezi kujilinda chenyewe?)
1.                  Angalia maneno ya mwisho ya fungu la 5: “Hawawezi kutenda uovu wala hawana uwezo wa kutenda mema.” Je, umewahi kusikia kwamba baadhi ya watu wanaogopa laana ya sanamu? (Mungu anasema kuwa hupaswi na wala huna cha kuogopa.)
1.                  Jambo gani linafanana na hilo katika zama za sasa? Kama nilivyokwishabainisha hapo awali, hakuna mtu hata mmoja ninayemfahamu anayekata mti, kuuchonga na kisha kuuabudu. (Mantiki ya Mungu ni kubwa kuliko kitu chochote kilichotengenezwa na wanadamu. Ukiwa unakitegemea kitu kilichotengenezwa na mwanadamu mwenzako, tofauti na kumtegemea Mungu, basi upo kwenye tatizo lile lile la kimantiki.)
A.                Soma Yeremia 10:6-7. Nani anayefanana na Mungu? (Hakuna mtu hata mmoja.)
1.                  Je, Mungu anastahili kuabudiwa nasi? (Ndiyo! “Hii ni stahili yako.” Watu wasiomwamini Mungu ni wapumbavu. Wanamnyima Mungu kile anachokistahili.)
A.                Bila shaka yote ambayo tumekwishayajadili hivi punde katika maswali haya machache ni dhahiri kwako. Kwa nini Yeremia anaandika kuyahusu? (Kwa sababu hayako dhahiri kwa watu wa Mungu. Wanaitegemea miti pamoja na vitu vingine walivyovitengeneza.)
1.                  Je, hii inaashiria nini kwetu kuhusu ugumu wa kutatua matatizo katika familia zetu na katika makanisa yetu? (Watu wengine hawana akili. Jibu liko wazi kuhusu kuabudu mti. Ndio maana jibu la matatizo mengi katika familia na kanisani pia liko dhahiri, lakini Mungu pamoja na Yeremia wanatakiwa kushughulika na watu wasioweza kuona mambo yaliyo bayana – vivyo hivyo kwetu pia.)
a.                   Tunapaswa kufanya nini katika hali zilizo dhahiri kabisa kama hizi? (Soma Yeremia 10:22. Tunatakiwa kuomba ili Mungu “arekebishe” hali.)
I.                   Hatari
A.                Soma Yeremia 26:1-3. Matumaini ya Mungu ni yapi? (Kwamba watu watakaposikia kile anachowaambia Yeremia kwa niaba ya Mungu, watageuka na kuuacha uovu wao.)
A.                Soma Yeremia 26:4-6. Mungu anawapatia watu uchaguzi. Achana na dhambi nawe utaokolewa dhidi ya janga, au endelea kutenda dhambi ili uwe mfano. Je, unadhani utafanya nini endapo utakabiliana na hizo chaguzo zilizo bayana kabisa?
A.                Soma Yeremia 26:7-8. Je, ni uchaguzi gani wa tatu ambao watu waliuchagua? (Kumnyamazisha Yeremia kwa kumuua.)
1.                  Hebu turejee mjadala wetu juu ya kutafuta suluhu ya tatizo katika familia au kanisani. Je, mara zote mambo yanakuendea barabara? (Kwa dhahiri, hapana, kama jinsi Yeremia anavyoonesha. Lakini, unatakiwa kuwa na uhakika kwamba unazungumza kwa ajili ya Mungu (unamzungumzia Mungu).)
A.                Soma Yeremia 26:9. Je, ungejisikiaje endapo ungekuwa Yeremia – watu wanakuzunguka huku wakipiga kelele kwamba unapaswa kufa?
            
A.                Soma Yeremia 26:10-11. Mashtaka gani yanatolewa dhidi ya Yeremia yanayomfanya astahili kufa? (Alisema mambo mabaya kuhusu mustakabali wa Yerusalemu.)
1.                  Unaichukuliaje mantiki ya mashtaka hayo? (Suala sio kusema ukweli, bali suala ni endapo ninafadhaishwa na kile unachokisema. Tunalo tatizo hili katika zama za sasa. Kiukweli watu hawaujali ukweli, kwa sababu ukweli ni chochote kile unachokiamini kuwa ni kweli. Badala yake, suala lililopo ni endapo mtu anafadhaishwa kwa kile unachokisema.)
A.                Soma Yeremia 26:12-15. Je, Yeremia anaonekana kuogopa? (Anazungumza kwa ujasiri!)
A.                Soma Yeremia 26:16. Je, kitendo hiki kinakutia hamasa? (Inaonekana kwamba watu hawa hawakuwa na matumaini yoyote. Lakini, Yeremia anazungumza kwa ujasiri na watu wanaguswa dhambi zao. Bila shaka Roho Mtakatifu yupo kazini.)
A.                Rafiki, tunapokabiliana na matatizo ambayo hatujui namna ya kuyatatua, tunapaswa kumgeukia Mungu kwa ajili ya kupata suluhisho. Mungu anatuambia kwamba katikati ya matatizo tunaweza kuwaambia watu wengine kuwa yeye ni mwema na mwenye kutenda haki! Je, utayageuzia matatizo yako kwa Mungu?

I.                   Juma lijalo: Uongofu wa Yosia.

No comments:

Post a Comment