SIKU YA KUTAMBUA HUDUMA YA MCHUNGAJI



Tarehe 17 Oktoba 2015, imetengwa na Kanisa la Waadventista wa Sabato ulimwenguni, kuwa siku ya kutambua mchango wa wachungaji wake wanaofanya kazi katika mazingira magumu na ya kujinyima. Huu ni wakati maalumu katika mwaka, wa kuonesha utambuzi na shukrani za mitaa, makanisa, na mshiriki mmoja mmoja kwa wachungaji wao ambao hutumia muda mwingi kuwahudumia waumini hao kiasi cha hata wengine kushindwa kuzihudumia familia zao inavyostahili. Wachungaji wetu licha ya kutoa mahubiri kila wakati, wamekuwa pia wakitembelea washiriki, makundi na makanisa, wakiwaombea, wakitoa ushauri wa kiroho na kifamilia, na huduma zingine mbalimbali za kijamii. 
Kanisa mahalia au mtaa uandae mhubiri atakayechambua namna mchungaji anavyojitoa mhanga katika kuwatumikia watu wa Mungu na jinsi waumini wanavyopasa kumtia moyo na kushirikiana naye. Miongoni mwa mafungu anayoweza kuyatumia ni kama; “Lakini, ndugu, tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao. Iweni na amani ninyi kwa ninyi. (1 Thess. 5:12, 13), na “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.” (Waeb. 13:7). Kwa kadri itakavyowezekana nyimbo za tukio hili ziendane na kutambua huduma inayotolewa na mchungaji. 
Hii ni siku ya kutambua jinsi mchungaji alivyotumia vipawa, muda, nguvu na mali zake katika kusaidia kusukuma maendeleo ya watu anaowasimamia kufikia hapo walipo sasa. Kwa wengine itakuwa siku ya kumtambua mchungaji aliyekubatiza, aliyefunga ndoa yako, aliyekuhubiria ukweli uliokuweka huru, au aliyefanya jambo maalumu la kukusaidia kimaisha. Hata kama ni mchungaji anayehudumu mbali na ulipo huu ndiyo wakati wa kuwasiliana naye na kumjulisha kuwa unathamini huduma aliyokutendea na unamuombea. Ni siku pia ya kutoa ushuhuda mbele ya familia ya mchungaji juu ya namna unavyoguswa na huduma yake, kwa wengine watakaokosa nafasi hiyo watatumia njia zingine za mawasiliano kufikisha ujumbe huo, kama mazungumzo ya simu, ujumbe mfupi wa maneno, kadi, barua, na mitandao ya facebook, au Whatsap. 
Katika siku hiyo chakula cha pamoja chaweza kuandaliwa na zawadi kadhaa zikatolewa kwa mchungaji na familia yake kama ishara ya kutambua mchango wake. Zawadi si lazima ziwe kubwa bali zilenge kurahisisha kazi zake mfano chombo cha usafiri au ukarabati mdogo wa chombo chake cha usafiri, uboreshaji wa ofisi ya mchungaji, au uboreshaji wa mazingira anapoishi, zinafaa sana katika juma hili. Licha ya kutoa zawadi ya vitu watakaojisikia kuwapatia familia ya mchungaji au mchungaji mwenyewe fursa fulani maalumu ambayo wamekuwa wakiikosa pia wanaweza kufanya hivyo. Fursa hizo ni kama ya kutembelea maeneo maalumu ya kiutalii, maeneo ya kihistoria ya Biblia (Israel n.k.), ama fursa ya kwenda kusoma nk. Waumini wanaweza kuandaa cheti au ngao ya kutambua mchango wa mchungaji wao ambapo yaweza kuandikwa hivi. 
CHETI CHA UTAMBUZI
Tunatambua mchango wa kujikana nafsi uliotolewa na [Jina la Mchungaji] na [Mke wa Mchungaji] na Familia yao, katika kusaidia kulijenga kanisa/mtaa ___________
Leo tarehe 17, Oktoba, 2015
Kwa kutambua kuwa mchungaji anazungukwa na majaribu mengi na ya kuwa yeye naye ni binadamu mwenye madhaifu mbalimbali, itakuwa jambo la muhimu siku hiyo au siku kadhaa kabla ya siku hiyo kuwa na maombi maalumu kwa ajili yake na familia yake. Pia kikundi maalumu cha viongozi wa kanisa waweza kupanga ziara nyumbani kwa mchungaji katikati ya juma ili kuisalimu familia, kuiombea na kuipa maneno ya faraja. Katika juma la kuelekea Sabato ya utambuzi wa huduma ya mchungaji somo maalumu linaweza kuendeshwa likisimamiwa na wazee wa kanisa kwa mashauriano na mchungaji wa mtaa na mkurugenzi wa wachungaji wa konferensi husika. Hebu kila mmoja shiriki kikamilifu kuifanya siku ya kutambua huduma ya Mchungaji kuwa yenye mafanikiko. Kila la heri na Mungu awabariki.
IMETOLEWA NA KATIBU WA WACHUNGAJI - STU

No comments:

Post a Comment