Somo La 10 | Kuangamizwa kwa Yerusalemu

Somo limetafsiriwa na Mgune Masatu

(Ezekiel 8, Yeremia 29, 37-38)
Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2011, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.
Utangulizi: Katika Yeremia 17:9 anasema kuwa “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?” Tunao uwezo mkubwa ajabu wa kuweza kujidanganya sisi wenyewe. Wale wanaomkataa Mungu wanayo hoja, wana sababu, kutokana na tabia yao ya kiovu. Yeremia aliwaona watu wakijiingiza kwenye tabia zenye vioja. Kwa upande mmoja walidai kuwa wanamfuata Mungu, na kwa upande mwingine walimkataa Mungu. Kwa nini tu wasimkatae Mungu na kuacha kujisingizia (kujidai)? Je, hili ndilo jambo tunalopaswa kuwa na wasiwasi nalo, kwa kuwa tunadai kwamba tunamfuata Mungu? Hebu tuchimbue somo letu la Biblia ili tujifunze zaidi!
I.                   Kisingizio
A.                Soma Ezekieli 8:9-11. Kitu gani kipo mbele? (Wazee wakifanya ibada inayoonekana kumtumikia Mungu.)
1.                  Kuna nini nyuma? (Vinyago na vitu vya kuchukiza.)
2.                  Ezekieli anapewa maono ya mambo yanayoendelea katika zama za Yeremia. Unawezaje kuelezea kile alichokiona Ezekieli? (Unafiki. Upande wa “mbele” unaonekana kuwa sahihi, lakini kinachoendelea nyuma ya pazia ni mbali sana na mambo sahihi.)
B.                 Soma Ezekieli 8:12. Wazee wanatoa sababu gani kutokana na tabia yao isiyo sahihi? (Sababu mbili. Sababu ya kwanza, ni kwamba kwa namna fulani Mungu haoni kile wanachokifanya. Sababu ya pili ni kwamba Mungu amewaacha.)
1.                  Ukweli ni upi? (Ni kinyume chake. Mungu anawaona, na Mungu amefadhaika sana. Badala ya kuwatelekeza, anawaadhibu kwa matumaini ya kurejesha mambo katika hali ya kawaida.)
2.                  Jiweke kwenye nafasi ya mmojawapo wa hawa wazee kwa kuvaa viatu vyake. Je, mtazamo wako wa mambo unakubaliana na kweli hizi? (Ndiyo. Ikiwa unadhani kwamba Mungu anapaswa kukutetea bila kujali chochote kile unachokifanya, basi mtafaruku unaoendelea unaweza kuhusianishwa na kitendo cha Mungu kukutelekeza.)
3.                  Ikiwa wazee wana maelezo yenye mantiki, kwa nini Mungu hana furaha kiasi hicho? (Kwa sababu wamekataa kumwamini Yeremia. Kuna njia mbili za kuliangalia jambo hili, na ikiwa utaliangalia kwa kuzingatia maonyo ya Yeremia, na maelekezo yaliyopo kwenye neno la Mungu kwa njia ya maandishi, wazee walipaswa kufahamu kuwa mtazamo wao wa mambo haukuwa sahihi.)
4.                  Vipi kuhusu wewe? Unapoyachunguza maisha yako, je, kujihesabia kwako haki kwa sehemu fulani kunatokana na kupuuzia maonyo ya Biblia?

II.                Kuishi kwa Kisingizio
A.                Soma Yeremia 37:1-2. Je, Mfalme Sedekia na washauri wake wanasikiliza kile anachokisema Mungu kupitia kwa Yeremia? (Hawatilii maanani anachokisema Mungu.)
B.                 Soma Yeremia 37:3. Kwa nini anaomba kuombewa?
1.                  Je, unawafahamu watu wanaofanana na mtu huyu? Hawatilii maanani kile anachowaambia Mungu, na kisha wanaomba kuombewa wanapojikuta kwenye matatizo?
a.                   Je, kitendo hiki ni kizuri au kibaya? Je, tunapaswa kujisikia ahueni kwamba hatimaye mfalme anaomba kuombewa?
b.                  Au, kuomba kuombewa ni kujidanganya zaidi?
C.                 Soma Yeremia 37:5-8. Zedekia alikuwa anategea nini? (Alidhani Misri itamwokoa. Mpango wake ulionekana kufanya kazi. Misri ilipotoka, Babeli ilijiondoa mahali ilipokuwa imezingirwa na Yuda.)
D.                Soma Yeremia 37:9-10. Hebu turejee swali linalohusu kumwomba Mungu wakati ulikuwa ukimpuuzia. Je, Mungu alijibu maombi ya Sedekia? (Ndiyo! Nadhani mara zote maombi ndilo jibu sahihi. Lakini, utaona kwamba Mungu habadiliki. Bado ana ujumbe ule ule ambao Sedekia amekua akiukataa.)
III.             Kuugeukia Ubaya Zaidi
A.                Soma Yeremia 38:2-3. Huu ni ujumbe ule ule wa Yeremia – jisalimisheni na acheni kushindana na Babeli. Endapo ungekuwa kiongozi wa Yuda, je, ungeupenda ujumbe huu?
B.                 Soma Yeremia 38:4. Nahisi nawe ulikuwa unafikiria jambo hilo hilo. Yeremia hawahamasishi wanajeshi na hatii hamasa morali ya watu. Unadhani Yeremia alitakiwa awe anafanya nini?
1.                  Je, kuna chochote cha kujifunza linapokuja suala la kuwashauri watu wanaokataa kuuacha uovu? (Ikiwa tuna uhakika kwamba tunao ujumbe wa Mungu, basi tunatakiwa kuung’ang’ania ukweli. Yeremia alikuwa hawaambii ujumbe “wenye kuwafurahisha,” alichokuwa anakisema kilikuwa ni maangamizi katika mipango ya viongozi kumpinga Mungu.)
C.                 Soma Yeremia 38:6. Je, ungependa kuzamishwa kwenye matope shimoni? (Ni jambo la kutisha.)
1.                  Je, tutarajie kuwa kwenye “matope” tunapozungumza dhidi ya uovu? (Ukisoma Yeremia 38:7-13 utaona kwamba Mungu anamhamasisha kiongozi, Ebedmeleki, kuingilia kati ili kumwokoa Yeremia dhidi ya kufa kwa njaa chini ya shimo.)
IV.             Nafasi ya Mwisho

A.                Soma Yeremia 38:14-15. Unalichukuliaje ombi la Mfalme Sedekia? Je, jibu la Yeremia lina mantiki? (Kwa dhahiri Mfalme amekanganyikiwa kuhusiana na endapo anapaswa kumsikiliza Yeremia.)
B.                 Soma Yeremia 38:16. Kwa nini mfalme aliapa kwa “siri” kiapo hiki kwa Yeremia?
C.                 Soma Yeremia 38:17-18. Hii inatufundisha nini kumhusu Mungu? (Ni mvumilivu. Bado anampa Sedekia njia ya kutokea. Bado ana matumaini.)
V.                Muda Umekwisha
A.                Soma Yeremia 39:1-2 na Yeremia 39:4-7. Wanao wameuawa, na hicho ndicho kitu cha mwisho kabisa kukiona maishani mwako. Fikiria jinsi mambo yalivyo kwa Mfalme Sedekia sasa?
B.                 Soma Yeremia 39:8-9. Mambo yote yametoweka. Yerusalemu imechomwa moto na watu wamechukuliwa mateka. Kuzitumainia sanamu na kuitumainia Misri kumewatendea nini watu wa Yuda?
1.                  Je, hii ni kanuni ya jumla inayotumika kwako, tunapoweka matumaini yetu kwa watu wengine na kwa vitu tulivyovitengeneza?
C.                 Soma Yeremia 39:11-12 na Yeremia 39:15-18. Utakumbuka kwamba Ebedmeleki aliingilia kati ili kumwokoa Yeremia dhidi ya kufa kwa njaa katika shimo la ghala. Kuna lipi la kujifunza kwa wale wanaosimama kwa ajili ya Mungu wakati usio na umaarufu? (Mungu anawaangalia watu wanaomtumikia.)
VI.             Kutenda kwa Ubora wa Hali ya Juu
A.                Umepata majanga maishani mwako na lawama zote ni juu yako kwa kuwa wewe ndio umeyasababisha. Unatakiwa kufanya nini?
1.                  Hebu tusome barua ambayo Yeremia aliituma kwa wale waliochukuliwa mateka Babeli. Soma Yeremia 29:4-6. Yeremia anatoa ushauri gani? (Jaribu kuishi maisha ya kawaida kwa kadri inavyowezekana. Endapo umeyachezea maisha, kamwe mambo yanaweza yasiwe kama ilivyotarajiwa yawe, lakini unatakiwa ujitahidi kuishi maisha ya kawaida.)
B.                 Soma Yeremia 29:7-8. Je, unatakiwa kufanya jambo gani jingine kwa wale waliokupatia maadili mema maishani mwako? (Watu wa Mungu wanaweza kuwadharau watu wa Babeli na kujaribu kuwaona kuwa ni watu wa hali ya chini. Lakini, Mungu anasema kuwa watu wake wanatakiwa kufanya kazi pamoja na watu wa Babeli ili kuyafanya maisha yawe bora zaidi kwa ajili yao wote.)
C.                 Soma Yeremia 29:10-11. Hii inamaanisha nini kwa watu wengi? (Kwamba watakufa wakiwa utumwani.)
1.                  Ni kwa jinsi gani ujumbe huu ni wa matumaini? (Watoto wao watarejea Yuda.)
2.                  Unawezaje kutumia somo hili maishani mwako endapo umefanya mambo yaliyosababisha majanga? (Weka matumaini yako katika kusaidia kuyafanya maisha ya watoto wako yawe bora zaidi. Jaribu kufanya mambo yawe ya kawaida kabisa sasa hivi kwa kadri uwezavyo, ili siku zijazo ziwe bora.)

D.                Rafiki, wanadamu wana uwezo mkubwa na wa ajabu wa kuweza kujidanganya wenyewe. Mwombe Mungu akuoneshe asili ya kweli ya moyo wako. Ikiwa umechelewa sana, na tayari umeshayaharibu maisha yako, mgeukie Mungu, jaribu kuyafanya maisha yawe ya kawaida kwa kadri inavyowezekana, na jitahidi kuwaandalia wanao maisha bora zaidi. Je, utajitoa kwa ajili ya hilo?

VII.          Juma lijalo: Agano.

No comments:

Post a Comment