NENO LA LEO - MTEGO ULIOWANASA WENGI

Ayubu 20:12-13, 27. "Ingawa uovu una tamu kinywani mwake, ingawa auficha chini ya ulimi wake, Ingawa auhurumia, asikubali kuuacha uende zake, lakini akaushika vivyo kinywani mwake;.......... Mbingu zitafunua wazi uovu wake, nayo nchi itainuka kinyume chake".

��Sitasahau mkasa uliomtokea dada mmoja aliyekuwa anatembea na mume wa mtu kwa muda mrefu, siku arobaini zilipofika, saa nane ya usiku wakiwa katikati ya tendo la kuvunja amri ya Mungu ya Usizini, walivamiwa na majambazi nyumbani kwa binti, katika purukushani za kujiokoa mwanaume akapigwa risasi ya kichwa na hatimaye mauti, na binti akavunjwa mguu kwa risasi.

��Japo huyo binti alifanikiwa kuitunza hiyo siri kwa miaka mingi, akidumu kuihujumu ndoa ya watu, kwa kuuficha utamu wa mapenzi chini ya ulimi wake,  siku ikafika neno la Mungu likatimia, Mbingu zikaufunua uovu wake, mume wa mtu kauwawa uchi wa mnyama kitandani pake, na yeye kujikuta hospitali alikopelekwa bila kujitambua akiwa na mguu uliovunjika unaosubiri kukatwa.

��Hata leo hii, kuna wengi wanaosoma ujumbe huu wakiwa katika mtego huu wa kuvinjari katika UOVU fulani kwa siri, wengine wamejiegesha kwa waume za watu, wengine kwa wake za watu, wengine ni wezi wa wachumba za watu, wengine kazi yao ni kudanganya na kuharibu mabinti na kuwabwaga, na majimama kuwaharibu vijana wa kiume kwa siri wakitumia mali zao.

��Rafiki hakuna uovu unaotendeka kwa siri utakaomshinda Mungu asiufunue, ukiona umefanikiwa, ujue Mungu anakuvutia muda ili UTUBU na Kuacha haraka, kabla hajaruhusu dhoruba itakayokuaibisha milele, iwe ni Ufisadi, uchonganishi, udokozi, unaruka ukuta kwenda kuzungurusha viuno kweye muziki wa dansi, unaua vitoto kwa kutoa mimba, ni mla rushwa au mtoa rushwa, iwe ya pesa au ya ngono nk, ACHA kabla neno la leo halijatimia au KABLA YA MTEGO KUFYATUKA NA KUKUNASA.

��Kumbuka Mwana wa Mungu alikuja duniani, na hatimaye kufa msalabani, ili kutukomboa kutoka katika kila mitego (dhambi), na kutuhakikishia uhuru baada kusamehewa makosa tuliyotenda. Huu ni wakati wa kushinda kwani hakuna ajuae ya Kesho.

NEEMA YA MUNGU IZIDI KUOGOZA NAFSI ZETU KATIKA USHINDI DAIMA - NAWATAKIA SIKU NJEMA.

Na Ev Eliezer Mwangosi.
Kwa mawasiliano zaidi na ushauri au maswali tumia: 0767210299, eliezer.mwangosi@yahoo.com.

No comments:

Post a Comment