Somo La 3 | Umoja Wa Injili

Somo limetafsiriwa na Mgune Masatu
(Wagalatia 2)
Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2011, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.
Utangulizi: Paulo anawasilisha umoja wa namna gani? Hadi kufikia hapa, anaonekana kupendelea zaidi kusema kwamba injili yake inatoka kwa Mungu moja kwa moja, na si kwa viongozi wa kanisa. Hiyo inaonekana kuwa njia ya ajabu katika kuufikia umoja! Yumkini sisi sio wajuzi kama Paulo. Huenda Paulo alijua kwamba alipaswa aendelee katika njia yake mwenyewe kuwafundisha Mataifa kama alivyoelekezwa na Mungu. Ni baada tu ya kuanzisha kazi yake ndipo aweze kwenda kwa viongozi wa kanisa kwa ajili ya wao kuidhinisha kazi yake. Hebu tusome kile anachokiandika Paulo ili tuone kama hiyo ndio njia aliyoitumia!
I.                   Miaka Mingi Baadaye
A.                Soma Wagalatia 2:1. Linganisha na Wagalatia 1:18-19. Paulo anataarifu kwamba miaka mitatu baada ya kuongoka kwake anatembelea Yerusalemu na ana mawasiliano machache sana na uongozi wa kanisa. Kisha miaka kumi na minne baadaye, anajitokeza ili kukutana na uongozi wa kanisa tena. Ikiwa ulikuwa unamshauri Paulo awe na umoja na uongozi wa kanisa, je, ungependekeza hii njia iliyotumika? (Nisingeshauri hivyo. Hii inaonekana kuwa kinyume na kile kinachopaswa kufanyika ili kuleta umoja.)
B.                 Soma Wagalatia 2:2. Kwa nini Paulo alijitokeza miaka kumi na minne badaye? (“Katika kuitikia ufunuo.” Mungu alimwambia awatembelee viongozi. Hiyo inaashiria kwamba hapo awali Mungu hakumwambia arudi Yerusalemu ili kuonana na kushauriana na uongozi.)
1.                  Unadhani Paulo angesafiri kwenda Yerusalemu endapo Mungu angekuwa hajamwelekeza kuwatembelea viongozi? (Sidhani. Ikiwa ulikuwa umepotea kwa miaka kumi na minne, na hudhani kwamba unahitaji kushauriana na uongozi, kwa nini basi ushauriane nao?)
2.                  Unadhani kwa nini Mungu alimsubirisha Paulo kwa muda mrefu?
II.                Mwendelezo Ule Ule?
A.                Soma 1 Wakorintho 1:10-12. Paulo anawezaje kuaminika anapojenga hoja ya umoja miongoni mwa uongozi, wakati yeye binafsi anafanya mambo yake mwenyewe miongoni mwa Mataifa angalao kwa muda wa miaka kumi na minne?
B.                 Soma tena Wagalatia 2:2. Kwa nini Paulo anasema kuwa aliamua kukutana na uongozi wa kanisa kwa faragha? (Aliogopa kwamba alichokuwa anakifanya kilikuwa ni sawa na kazi bure.)
1.                  Unadhani hiyo inamaanisha nini?

2.                  Soma Wagalatia 1:6-8. Paulo hana mashaka na namna anavyowasilisha injili, hivyo basi yawezekana Paulo alikuwa anazungumzia jambo gani anaposema kuwa alihofia kwamba kutanga kwake kote kulikuwa ni kazi bure?
C.                 Haya ni maswali magumu. Paulo anawezaje kuwa anatangaza umoja kwa kukaa mbali, na ni kwa jinsi gani Paulo anaweza kudhani kuwa yumkini alikuwa akitanga bure? Je, inawezekana kwamba tunaliangalia jambo hili kwa njia isiyo sahihi?
D.                Soma 1 Wakorintho 1:18-19. Je, mara zote Mungu anatenda kazi kwa namna inayoleta mantiki kwetu?
1.                  Ikiwa Paulo yuko sahihi kwamba anahubiri injili ya kweli, hilo fundisho sahihi linaweza kuonekanaje kwa wale walioikataa neema? (“Upumbavu.”)
2.                  Tafakari jambo hili kidogo. Kituo cha usaidizi wa sheria ya Musa kilikuwa Yerusalemu. Endapo Paulo angewasilisha mara moja injili yake ya neema kwa watu wa Yerusalemu, kitendo hicho kingepokelewaje? (Soma Matendo 9:23-25 na Matendo 22:17-21. Baada ya uongofu wake, Paulo alidhani kwamba anastahili sana kuwasilisha injili kwa Wayahudi waliofanya naye kazi. Tunaona sio tu kwamba Mungu hakukubaliani naye na kumpeleka kwa Mataifa, bali pia Wayahudi walijaribu kumwua. Jambo la mwisho ambalo Paulo alipaswa kulifanya ili kuutangaza “umoja” ilikuwa ni kuwasilisha injili yake kwa Wayahudi kule Yerusalemu.)
a.                   Mara baada ya Paulo kukataliwa na washiriki wa kanisa Yerusalemu, tayari hilo liliathirije kwa kiasi kikubwa kazi yake? (Endapo Paulo asingekuwa amefanya kazi peke yake kwa miaka yote hiyo, angewasilisha hoja yake (inaonekana hivyo) kwa makundi ya watu Yerusalemu, angekataliwa (au kuuawa) na hiyo ingehitimisha kazi yake bado ikiwa changa.)
E.                 Soma Wagalatia 2:3-5. Jambo gani linaleta mtafaruku? (Tohara inatajwa.)
1.                  Njia aliyoitumia Paulo inautangazaje mtazamo wake? (Kifungu cha 5 kinathibitisha kwamba Paulo hadhani kuwa ujumbe wake wa injili ni potofu. Badala yake, tunaona kwamba kwa kukutana na baadhi ya viongozi kwa faragha, aliweza kuelezea mambo aliyokuwa akiyatenda Mungu kupitia kwake. Hii inaelezea kile kinachoonekana kuwa njia ya ajabu ya Paulo. Anakaa mbali kwa muda mrefu ili muda mwafaka uweze kufika, anakwenda kwa viongozi na ujumbe wake kwa mkakati maalum na sio kwa makundi ya watu.)
III.             Majukumu Tofauti
A.                Soma Wagalatia 2:6. Chukulia kwamba huyu ni mchungaji wako akiandika juu ya uongozi wa madhehebu yake. Unaweza kudhani kwamba yeye ni bingwa wa umoja?
1.                  Sababu ya Paulo kuandika kauli hiyo inayoonekana kama ya uasi ni ipi? (Kwa mara nyingine, anao ujumbe aliofundishwa na Yesu, sio ujumbe aliofundishwa na wanadamu wengine.)

B.                 Soma Wagalatia 2:7. Unaweza kuona ujumbe wa umoja kwenye hii kauli? (Ukiangalia kwa mtazamo mpana, unaweza kuuona umoja. Paulo anasema kuwa anayo sehemu ya ujumbe wa kupelekwa kwa watu (Mataifa) na Petro anayo sehemu nyingine ya ujumbe wa kupelekwa kwa watu (Wayahudi).)
C.                 Soma Wagalatia 2:8. Nani anawajibika kwa mgawanyo wa majukumu ndani ya kanisa? (Mungu. Kama ambavyo ujumbe wa Paulo unatoka kwa Mungu, vivyo hivyo ugawaji wa majukumu unatoka kwa Mungu.)
1.                  Unawezaje kutumia njia hii kufikia masuala ya umoja leo? Kwa mfano, katika madhehebu yangu, kwa sasa kuna mgogoro juu ya wanawake kuwekewa mikono. Vipi kama wale wanaoshadadia uwekewaji mikono watasema kwamba Mungu ndiye aliyeelekeza msimamo wao, na kwamba Mungu ameweka mpango kuwa katika baadhi ya sehemu hapa duniani wanawake wawekewe mikono kuwa wachungaji na maeneo mengine ya dunia hii wasiwekewe? Je, mambo hayo yanafanana?
a.                   Kumbuka kwamba tulipojadili jinsi kanisa la awali lilipokabiliana na mgawanyiko, uamuzi ulifikiwa wa kuizingatia kazi ya Roho Mtakatifu? (Angalia Matendo 15:12-13.)
D.                Soma Wagalatia 2:9. Paulo anasema kuwa nini kilithibitisha njia yake na kilithibitisha kwa msingi gani? (Hatimaye, Paulo anatuambia kwamba “nguzo” za kanisa la awali zilithibitisha kazi yake. Hata hivyo, utaona kwamba msingi wa uthibitisho ni “neema aliyopewa” Paulo. Tunachoona ni kwamba viongozi wa kanisa walikiri mwelekeo ambao Mungu anauongoza.)
E.                 Soma Wagalatia 2:10. Utakumbuka kwamba jambo la kwanza kabisa ni tohara. Je, viongozi wa kanisa wanaomba mabadiliko yoyote kwenye mafundisho ya Paulo? (Hapana.)
1.                  Je, unakumbuka kwamba tangu mwanzoni mwa barua yake kwa kanisa la Galatia, Paulo amekuwa akijenga hoja juu ya mamlaka ya mafundisho yake? Sasa anataarifu kwamba Mungu ndiye chanzo cha mafundisho yake na nguzo za kanisa zinakubaliana naye! Vipi kama nguzo za kanisa lako hazikubaliani na upande wako katika mgogoro wa kimaandiko?
2.                  Unadhani kwa nini viongozi wa kanisa walimwambia Paulo “awakumbuke maskini?” Kati ya mambo yote ambayo wangeweza kumwomba Paulo, je, hili linaonekana kama ombi lisilo la kawaida? (Ukosoaji halisi wa kuhesabiwa haki kwa imani ni upi? Unawaruhusu watu kuendelea kulisha tamaa zao za ubinafsi. Kuwasaidia watu wengine ni kielelezo cha moyo wa kuwajali. Na kwa kuongezea, maskini wanaojadiliwa ni Wakristo wa Kiyahudi. Kwa kuwa na Mataifa wakiwasaidia Wayahudi, kitendo hiki kitasaidia uwepo wa umoja.)
IV.             Kuonyesha Dhamira/Kusema Ukweli
A.                Soma Wagalatia 2:11-12. Nini kilimsababisha Petro atangaze msamaha kwenye uamuzi wake wa kuunga mkono mitazamo ya Paulo? (Ushawishi wa makundi!)

1.                  Fikiria migogoro ya kimaandiko unayoizingatia sana. Kwa kiwango gani uamuzi wako unatokana na kile ambacho watu wanaokuzunguka wanakifikiria? Kwa kiwango gani uamuzi wako unatokana na kile kinachofundishwa na Biblia?
B.                 Soma Wagalatia 2:13. Ushawishi wa makundi (makundi rika) una nguvu kiasi gani? (Inaonekana kwamba ni Paulo pekee ndio anaushinda ushawishi huo.)
C.                 Soma Wagalatia 2:14. Changanua hoja ya Paulo. Je, imejengwa kwenye Biblia? Unaweza kuiweka kwenye kundi gani? (Paulo anajenga hoja kwamba Petro ni mnafiki! Anabainisha kwamba Petro alikuwa hafuati desturi za Kiyahudi. Hivyo, itakuwa ni unafiki kwa Petro kuwalazimisha Mataifa kufuata desturi za Kiyahudi.)
1.                  Kwenye migogoro ya kimaandiko, je, tunapaswa kujenga hoja kama hizo ili kujenga umoja? (Tutakomea hapa kwenye hoja ya Paulo, lakini katika kifungu kinachofuata anajenga hoja iliyojengwa juu ya Biblia.)
D.                Rafiki, unaichukuliaje njia ya Paulo kwa mustakabali wa umoja wa kanisa? Kwa nini usiombe kwamba Mungu akusaidie uione njia madhubuti ya kuleta umoja kwa kanisa?

V.                Juma lijalo: Kuhesabiwa Haki kwa Imani Pekee.

No comments:

Post a Comment