Somo La 8 | Uongofu Wa Yosia

Somo limetafsiriwa na Mgune Masatu

(2 Mambo ya Nyakati 33-35, 2 Wafalme 23)
Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2011, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.
Utangulizi: Sulemani anasema kuwa watu wenye busara, kama ilivyo kwa watu wapumbavu na wajinga, wote wanakufa na kuwaachia watu wengine mali zao. Zaburi 49:10. Maishani tuko na watu wa aina mbalimbali wanaosababisha mambo tofauti tofauti kututokea. Yosia alikuwa mtu wa Mungu, lakini maisha yake machanga yalikuwa na msukosuko, na aliuawa vitani katika umri mdogo. Mambo haya yanaleta mantiki yoyote? Hebu tuchimbue somo letu la Biblia ili tuone kile tunachoweza kujifunza!

I.                   Asili ya Familia (Jamii)
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:1-3. Utagundua kwamba Manase alikuwa na umri wa miaka 12 alipoanza kutawala (alipotawazwa kuwa mfalme). Je, umri huo unatosha kufanya maamuzi sahihi kwa Mungu? (Alitawala kwa muda wa miaka 55. Kuna wakati aliwajibika kwa haya maamuzi ya kutisha.)
1.                  Manase alikuwa na baba wa namna gani? (Baba yake alikuwa Hezekia, mmojawapo wa mashujaa wa Mungu.)
1.                  Unadhani kwa nini Manase aliugeukia uovu?
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:9-11. Matokeo ya Manase kuuendeleza uovu ni yapi? (Jeshi la Ashuru lilimchukua mateka na kumdhalilisha.)
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:12-13 na 2 Mambo ya Nyakati 33:15-17. Ikiwa tumeiacha njia ya Mungu, je, tunapaswa kuwa na wasiwasi juu ya kilichomtokea Manase?
1.                  Au, je, tuseme kwamba endapo mwisho utaishia kuwa mzuri, basi tutataka kupitia chochote kile ambacho Mungu anakiruhusu?
1.                  Je, “minyororo” na “pingu” (2 Mambo ya Nyakati 33:11) ni mfano wa “upendo mzito?”
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:21-24. Je, uovu huu umeviruka vizazi kadhaa? Tunaye Hezekia ambaye ni mfalme mzuri, Manase ambaye ni mfalme mbaya ambaye anabadilika na kuwa mzuri, na kisha mwovu Amoni kama mfalme.
1.                  Ikiwa wafalme wabaya wanaweza kuwa na wana wema na wafalme wazuri wanaweza kuwa na wana waovu, je, jambo hilo linaeleza nini kuhusu mipaka ya malezi?
1.                  Soma Kutoka 20:5-6. Mafungu haya yanaashiria nini kuhusu wema na uovu kutoka kizazi hata kizazi? (Naamini kuwa malezi yanaleta tofauti kubwa. Wazazi wanaweza kuwabariki au kuwadhuru watoto wao kutokana na matendo yao. Hata hivyo, 2 Mambo ya Nyakati 33 inatuambia kuwa kuna ushuhuda wa pekee usioendana na nadharia hiyo.)
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:1-2. Walitunza vitabu vya historia - 2 Mambo ya Nyakati ni kitabu cha historia. Ikiwa Yosia alisomewa historia ya wafalme, je, anatakiwa kuhitimisha nini? (Kuna uhusiano kati ya kumtii Mungu na maisha bora.)
1.                  Vipi kuhusu asili ya familia yako? Je, unaweza kuona jambo lile lile ambalo Yosia aliliona?
I.                   Yosia
A.                Soma tena 2 Mambo ya Nyakati 33:24-25. Endapo ungekuwa Yosia, je, ungetumia muda wako kusoma historia, au ungejihusisha zaidi kuhusu mambo yaliyokuwa yanaendelea katika kipindi cha maisha yako? (Baba yake aliuawa, na kisha watu wakawaua wauaji na kumweka Yosia madarakani! Hizi zilikuwa nyakati za machafuko.)
1.                  Ukipitia mafungu tuliyoyasoma, utaona kwamba katika kipindi kirefu cha maisha ya Yosia mfalme mzuri alikuwa akitawala. Manase alimfuata Mungu katika nyakati za mwisho za uhai wake. Sehemu hii ya mwisho ni miaka sita ya kwanza ya maisha ya Yosia. Babaye Yosia ambaye alikuwa mwovu alitawala kuanzia kipindi ambacho Yosia alikuwa na umri wa miaka sita hadi minane. Je, Yosia bado ni mdogo sana kiasi cha kutotambua kwamba nyakati za machafuko ziliendana na babaye mwovu kuwa mfalme?
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:3. Kama unadhani kuwa palikuwepo na athari, je, machafuko hayo yalikuwa na athari gani kwa Yosia? (Mara kwa mara watu humrudia Mungu katika nyakati za taabu. Fungu linatuambia (kwa kutumia hesabu ndogo) kwamba Yosia alikuwa na umri wa miaka 16 wakati alipomtafuta Mungu.)
A.                Katika somo lililopita katika mfulilizo wa masomo haya tulijifunza matukio yaliyotokea katika 2 Mambo ya Nyakati 34:4-15. Kwa ufupi, Yosia alivunjavunja, kuzisagasaga, na kuchoma kila kitu kilichohusiana na ibada ya sanamu. Kisha alikarabati na kujenga hekalu la Mungu. Katika kipindi hicho cha ukarabati, kitabu cha torati kilipatikana. Hebu tusome 2 Mambo ya Nyakati 34:18-19. Kwa nini Yosia aliyararua mavazi yake aliposikia neno la Mungu likisomwa mbele yake kwa mara ya kwanza kabisa? (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:20-22. Yosia alitambua kuwa watu walikuwa wanakiuka maelekezo ya Mungu. Kutokana na kutokutii huku, Yosia aliujali sana (aliogopa) mtazamo wa Mungu kwa watu.)
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:23-25. Hulda nabii mke ana ujumbe maalum kwa Yosia – kwamba maafa yanakuja kwa sababu watu hawakumfuata Mungu.)
1.                  Endapo ungekuwa Yosia, je, mambo gani yangekuwa yanaendelea kukupitia mawazoni mwako? (Kimsingi, hiki ndicho alichokuwa anakiogopa. Yumkini mwitiko wake ni kwamba, “Hili si kosa langu! Sikuwa ninafahamu. Mimi ni mtu mwema.”
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:26-28. Mungu anao ujumbe mwingine kwa Yosia. Angalia anachokibainisha Mungu kuhusu Yosia na kile asichokibainisha. Mungu aliacha jambo gani? Unadhani kwa nini Mungu aliliacha? (Mungu anaubainisha mtazamo wa Yosia, Mungu habainishi kazi yote ambayo Yosia amekuwa akiifanya katika kuangamiza sanamu na kulijenga upya hekalu.)
1.                  Kuna lipi la sisi kujifunza katika zama za sasa? (Mungu anajali sana mitazamo yetu.)
A.                Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:29-33. Ikiwa Yosia aliahidiwa kuwa hatashuhudia maafa, kwa nini alifanya hivi? (Kwa sababu ya mtazamo wake. Alitaka kuyaendeleza mapenzi ya Mungu pamoja na watu. Hakuwepo tu kwa ajili ya kuyaokoa maisha yake mwenyewe.)
A.                Soma 2 Wafalme 23:29-30. Tulijadili mada hii pia katika somo la awali. Shujaa mkuu wa Mungu, Yosia, anauawa na Farao-neko katika vita visivyokuwa na umuhimu. Je, unawafahamu watu wema waliokufa mapema sana kabla ya muda?
1.                  Unadhani kwa nini Yosia alifariki katika hivi vita? Kwa nini Mungu hakumlinda? (Nadhani hii inakwenda nyuma zaidi kwenye ahadi aliyopewa katika 2 Mambo ya Nyakati 34:26-28, kwamba Mungu hatamruhusu ayaone maafa yaliyokuwa yanaijia nchi yake.)
a.                   Hebu tutafakari jambo hili kidogo. Yosia alikuwa mtu mwema maishani mwake mwote. Lilikuwa kosa la nani kwamba maisha yake yalikatishwa akiwa bado mdogo? (Ilikuwa ni kosa la watu waovu waliotangulia mbele yake.)
a.                   Hiyo inatufundisha nini kuhusu watu wema kuteseka na kufariki? (Mara nyingi matatizo yetu huwa tunajisababishia wenyewe. Lakini, Yosia alifariki kwa sababu ya dhambi za watu wengine. Hili ndilo tatizo la kuishi kwenye ulimwengu uliojaa uovu.)
a.                   Vipi kuhusu wajibu wa Mungu katika jambo hili? Je, Mungu angeweza kumwacha Yosia aishi maisha marefu na yenye mafanikio, na kisha kurejea katika wakati muafaka katita tarehe ya uangamivu wa taifa? (Huu ndipo wakati ambao mara kwa mara wanadamu wanaurejea, tunatilia shaka na kujenga hoja kwamba kwa nini Mungu hakutenda mambo kwa njia nyingine tofauti. Tunatakiwa tu kutumaini na kuyaamini maamuzi ya Mungu.)
1.                  Hebu tuangalie jambo hili kwa mtazamo mwingine. Soma 2 Mambo ya Nyakati 35:20-22. Je, hii inaashiria dosari ya aina fulani kwa Yosia kwa kifo chake? (Ndiyo. Tunaweza kuelewa kwa nini Yosia hakuweza kufikiria kuwa Farao-neko alikuwa mjumbe wa Mungu. Lakini Neko alikuwa na ujumbe kutoka kwa Mungu kama inavyooneshwa kwenye matukio yaliyofuatia. Nadhani hitimisho ni kwamba kuna mambo mengi sana katika matukio yanayotutokea maishani. Uamuzi wetu mkubwa ni kuwa na mtazamo wa kumtumaini Mungu na kulitii neno lake.)
I.                   Maelezo ya Hezekia
A.                Soma 2 Wafalme 20:1-3. Utakumbuka kwamba tulipochunguza asili ya familia ya Yosia, Hezekia alikuwa babu wa babu yake na alikuwa mtu mwema. Hezekia ana hoja gani, kwamba maisha yake yasikome? (Kwamba yeye ni mtu mwema. Hiki ndicho haswaa ambacho tumekuwa tukikijadili kwamba ni jambo la kufikirika, watu wema wanapaswa kuwa na maisha mema.)
A.                Soma 2 Wafalme 20:4-6. Je, umetiwa moyo? Unamwambia Mungu kwamba ulikuwa na umeendelea kuwa mtu mwema, na Mungu anayaongeza maisha yako na kuilinda kazi yako na nchi yako katika kipindi chote cha maisha yako? (Hivyo ndivyo haswaa tunavyotamani mambo yawe tunapomtumaini Mungu.)
A.                Soma 2 Wafalme 20:12-13. Je, unapenda kuwaonyesha watu vitu vizuri ulivyonavyo? Je, unaonyesha mali zako nzuri ulizonazo kwa wageni?
A.                Soma 2 Wafalme 20:14. Mfalme Hezekia haonekani kutatizwa anapowaonesha mawakala wa Mfalme wa Babeli dhahabu yake. Kwa nini? (Babeli ilikuwa nchi ya mbali, na Mungu aliahidi kumlinda (2 Wafalme 20:6).)
A.                Soma 2 Wafalme 20:15-18. Kama tunavyofahamu kutokana na kujifunza habari za Yeremia, Babeli ni tishio la karibu. Hatimaye Babeli iliiangamiza Yerusalemu pamoja na hekalu. Angalia tena mpango halisi wa Mungu kwa ajili ya kifo cha Hezekia, na jinsi kuongeza muda wa kuishi wa Hezekia kulivyobadili historia. Je, tunapaswa kufikia hitimisho gani?
A.                Rafiki, sote tunadhani kwamba maisha yetu ni ya muhimu sana – na kimsingi ni ya muhimu kwetu. Lakini, katika mpango mzima wa maisha sisi si wa muhimu kiasi hicho. Linapokuja suala la mkono wa Mungu kwa ajili ya mstakabali wetu tunatakiwa kumtumaini. Je, utafanya uamuzi wa kuyatumaini mapenzi ya Mungu sasa hivi kwa ajili ya maisha yako?

I.                   Juma lijalo: Nira ya Yeremia.

No comments:

Post a Comment